Subscribe For Free Updates!

We'll not spam mate! We promise.

Friday 29 January 2016

Rais Magufuli amteua Julian Banzi Raphael kuwa Naibu Gavana wa Benki Kuu ya Tanzania



Rais Magufuli amteua Julian Banzi Raphael kuwa Naibu Gavana wa Benki Kuu ya Tanzania

Thursday 21 January 2016

SSRA yazindua mfumo wa kielektroniki kupokea malalamiko




Mkurugenzi wa Utafiti, Tathmini na Sera, Ansgar Mushi.Mkurugenzi wa Utafiti, Tathmini na Sera, Ansgar Mushi.

 MAMLAKA ya Usimamizi na Udhibiti wa Sekta ya Hifadhi ya Jamii (SSRA) imeanzisha utaratibu mpya wa kupokea na kushughulikia malalamiko ya wanachama kwa kutumia mfumo wa Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA).
Kwa watumiaji wa simu za mkononi, huduma hii hupatikana kwenye Google play kwa jina la SSRA. Mwenye malalamiko anaweza kutembelea tovuti ya www.ssra.go.tz na kutoa maoni kwenye sehemu iliyoandikwa malalamiko na maoni.
Akizungumza na waandishi wa habari jijini Dar Es Salaam leo, Ansgar Mushi, Mkurugenzi wa Utafiti, Tathmini na Sera, amesema kuwa uanzishwaji wa mfumo huo ni moja ya hatua mbalimbali ambazo zimekuwa zikichukuliwa na SSRA katika kulinda na kutetea masilahi ya wanachama.
“Uanzishwaji wa mfumo huu ni moja ya hatua mbalimbali ambazo zimekuwa zikichukuliwa na Mamlaka katika kulinda na kutetea masilahi ya wanachama kwa mujibu wa sheria ya Mamlaka ya Usimamizi na Udhibiti wa Sekta ya Hifadhi ya Jamii Na. 8 ya mwaka 2008 iliyorekebishwa kwa sheria  Na. 5 ya mwaka 2012,” amesema Mushi.
Utaratibu huu wa kielektroniki umeanzishwa ili kumrahisishia mwanachama au mwananchi yeyote kutoa malalamiko  au maoni ya kuboresha sekta hii kwa maendeleo ya jamii  akiwa mahali popote kwa muda muda wowote kuhusu masuala ya sekta ya hifadhi ya jamii.
Mwanachama akishaingiza taarifa zake binafsi kama jina lake la kwanza, la kati na la ukoo, anuani ya posta, namba ya simu, namba ya uanachama na makazi ya mlalamikaji, mfumo hutoa namba ya kumbukumbu kwa mlalamikaji.
Taarifa binafsi za mlalamikaji husaidia kumtambua na kufanya mawasiliano na mwanachama mwenye tatizo. Kupitia Idara ya Utekelezaji na Uandikishaji mamlaka hupokea taarifa za wanachama na na malalamiko yaliyoingizwa kwenye mfumo kwa ajili ya kuyafanyia kazi kwa kufuatilia na kuwasiliana na mwanachama huyo kwa kupitia taarifa zake alizosajilia  kwenye mfumo wa kielektroniki.
“Kwa ujumla mawasiliano kati ya wananchi na Mamlaka yamerahisishwa kwa matumizi ya simu za mkononi kwa njia zilizoorodheshwa hapo juu. Pia Mamlaka ina utaratibu wa kuwasiliana na wadau kwa kutumia ujumbe ufupi (sms)  na barua pepe pamoja na namba ya simu ya 0762440706 ambayo inaingiza ujumbe wowote moja kwa moja kwenye mifumo ya kielektroniki,” ameongeza
Mushi amewataka wanachama kudumu kwenye mifuko yao ya kijamii hasa kipindi mwanachama anapoajiriwa na kampuni nyingine sababu kuna faida nyingi mwanachama akidumu kwenye mfuko wa hifadhi ya jamii.
“Kuna faida mwanachama anapodumu kwenye mfuko wa hifadhi ya jamii, mwanachama anapochangia kwenye mfuko hupata faida ya 2.7 ya mchango wake kwa mwaka. Anapodumu kwenye mfuko mmoja hadi kustaafu kwake ana uhakika wa kupata kiinua mgongo kinachoridhisha kuliko yule anayehama sababu anaanza moja,” amesema
Akijibu swali la mwandishi wa habari juu ya mwamko wa wananchi kujiunga na mifuko ya kijamii, amesema wananchi wengi wanakosa fursa ya kujiunga mifuko ya hifadhi ya jamii kutokana na sheria zilizowekwa kubana wananchi ambao hawajaajiriwa, ingawa hivi karibuni mifuko ya kijamii imejitahidi kulegeza sheria na kuruhusu wasioajiriwa kujiunga na mifuko ya hiyo.
Mushi amewataka wanachama wa mifuko ya hifadhi ya jamii na umma kutumia huduma hii kwani ni rahisi kutumia, ina uwazi na haihitaji mwanachama  au mdau kufika katika ofisi za mamlaka; inaokoa muda, nauli na kuboresha huduma kwa wanachama.

Na Regina Mkonde 

Serikali yapongezwa kufuta mfumo wa GPA

Wanafunzi wa Shule ya Sekondari wakiwa katika Mtihani.
Wanafunzi katika Mtihani 

SHIRIKISHO la Wamiliki wa Shule na Vyuo Binafsi nchini (TANGOSCO) limeipongeza Serikali kwa  kuondoa mfumo wa GPA na kurejesha madaraja katika matokeo ya mitihani kwenye shule za sekondari, hasa kwa kidato cha pili na cha nne.
Amesema mfumo huo umedumaza kiwango cha elimu na kushusha viwango vya wanafunzi kwa sababu wamekuwa wanasukumwa kupanda madarasa bila ya kuzingatia ufaulu wao.
“Waziri ameitendea haki jamii ya kitanzania kwa kuurudisha mfumo unaoeleweka na kukomaza viwango vya elimu nchini, hususani (katika) kipindi hiki ambacho nchi yetu imekuwa ya mwisho kwenye ukanda wa Afrika Mashariki katika kutoa wahitimu wenye wenye elimu bora. Pia wasomi wetu hawana viwango vizuri vya kupambana kwenye soko la ajira la nje ya nchi,” amesema na kuongeza:
“Wanafunzi wengi wa kidato cha pili wanaingia kidato cha tatu ingawa hawana ufaulu mzuri. Wanasukumwa ili mradi wawe wameingia kidato cha tatu. Hali hii ni sawa na kuhujumu jitihada za wazazi na walezi. Wazazi wanajitoa kusomesha watoto wao ili wapate elimu bora. Kitendo cha mwanafunzi kumaliza shule ilhali hana elimu yenye kiwango itakayomsaidia kushindana kwenye soko la ajira ni sawa na kumhujumu mzazi.”
Wadau wa elimu, hasa wamiliki wa shule na vyuo binafsi nchini, wamekuwa wanalalamikia mfumo wa GPA tangu ulipoanza kutumika katika miaka mwili ya mwisho ya utawala wa Rais Jakaya Kikwete.
Wanadai kwamba matumizi ya mfumo wa GPA yamerudisha nyuma maendeleo ya wanafunzi kwa kuwadekeza na kupunguza juhudi za kujifunza, kwa sababu hata waliofeli hujumuishwa na waliofaulu.
Vile vile, wanasema mfumo wa GPA haukidhi viwango vya soko la ajira za nje ya nchi. Baadhi yao wamekuwa wanasema GPA ni sawa na kupanua magoli ili timu inayoshindwa kufunga magoli ipate ifunge kirahisi.
Mwanzoni mwa wiki hii, Profesa Joyce Ndalichako, Waziri wa Elimu na Ufundi Stadi, amefuta mfumo wa GPA na kutaka Baraza la Mitihani la Taifa lirejeshe mfumo wa zamani wa kutumia madaraja kutangaza matokeo ya mitihani.
Hata hivyo, wakati TANGOSCO inampongeza waziri, tayari matokeo ya kidato cha pili ya mwaka jana yalikuwa yameshatolewa kwa mfumo wa GPA.
Naye Fidelis Mwampoma, mwenyekiti wa wakuu wa shule zisizo za serikali, alisema wazazi wengi hupeleka watoto wao shule za binafsi kwa sababu wanaamini kuwa ndizo hutoa elimu bora, na kwamba serikali ya awamu ya nne ilipoanzisha mfumo wa GPA ililenga kukomoa shule za binafsi kwa kuwa zinafanya vizuri, ili zifanane na za serikali katika ubora wa elimu.
Alisema pia kwamba serikali inapobadilisha mifumo kila mara inachangia kudumaza elimu na kupoteza dira ya elimu nchini. Aliitaka iige mfumo wa elimu wa Kenya ambao umedumu kwa muda mrefu, jambo lililochangia nchi hiyo kuwa na viwango vizuri vya elimu ikilinganisha na viwango vya Tanzania.
“Kitendo cha Serikali kubadilisha mifumo kila mara kimechangia kushusha kiwango cha elimu, mfano mzuri ni Kenya. Imedumu kwenye mfumo wa elimu ulioachwa na mkoloni lakini hadi sasa ina viwango vizuri na wahitimu wake wanafanya vizuri kwenye soko la ajira,” alisema Mwampoma.
Mwampoma aliitaka serikali iboreshe mazingira ya elimu na waalimu kwani ili elimu bora ipatikane, ni lazima waalimu waandaliwe masilahi na mazingira mazuri ya kazi.

Anaandika Regina Mkonde 

Saturday 2 January 2016

VIWANGO VYA UFAULU (GRADE RANGES) ZA MITIHANI HAZIJABADILIKA



VIWANGO VYA UFAULU (GRADE RANGES) ZA MITIHANI HAZIJABADILIKA

Baraza la Mitihani la Tanzania limekuwa likipigiwa simu na watu mbalimbali wakiomba ufafanuzi kuhusu taarifa zinazosambazwa kwenye mitandao ya kijamii kuwa limebadilisha Viwango vya Ufaulu (Grade Ranges).

Baraza la Mitihani la Tanzania linapenda kuwajulisha watahiniwa na umma kwa ujumla kuwa taarifa hizo ni za UONGO na zinalenga kupotosha umma na kuleta taharuki.

Hivyo, Baraza linaomba umma kuzipuuza taarifa hizo kwa kuwa Baraza halijafanya mabadiliko yoyote kuhusu Viwango vya Ufaulu vinavyotumika sasa.


Imetolewa na,


AFISA HABARI NA UHUSIANO


Chanzo: www.necta.go.tz

CUF: Hatutoshiriki sherehe za Mapinduzi

Naibu Katibu Mkuu wa CUF Ismail Jussa
                                                    Naibu Katibu Mkuu wa CUF Ismail Jussa

VIONGOZI wakuu wa Chama cha Wananchi (CUF) hawatashiriki shughuli za kiserikali zilizopangwa kwa ajili ya maadhimisho ya miaka 52 ya Mapinduzi ya Zanzibar, kutokana na serikali iliyopo kutokuwa na ridhaa ya Wazanzibari. Anaandika Jabir Idrissa … 
Taarifa iliyotolewa leo na Kurugenzi ya Habari na Mawasiliano na Umma ya chama hicho imesema hatua hiyo inatekelezwa katika kuzuia raslimali za wananchi kutumika vibaya ikiwemo kuendekeza uongozi wa serikali usiohalalika kisheria na kikatiba.
Kwa mujibu wa taarifa hiyo kupitia vyombo vya habari, hata Maalim Seif Shariff Hamad, Katibu Mkuu wa CUF na mwanasiasa aliyegombea urais wa Zanzibar katika uchaguzi mkuu wa Oktoba 25, ambao ulihujumiwa kwa makusudi, hatahudhuria sherehe hizo zitakazofikia kilele Januari 12, kwenye Uwanja wa Amaan, mjini Zanzibar.
Taarifa imesema chama hicho kimekuwa kikishiriki sherehe za Mapinduzi tangu kilipoanzishwa kwa kuwa kinatambua umuhimu wa siku hiyo ambayo ilikuwa ndio imeipatia Zanzibar jamhuri chini ya kiongozi wake wa kwanza, Mzee Abeid Amani Karume.
Lakini, taarifa imeeleza, malengo ya Mapinduzi hayo yalikuwa ni pamoja na Zanzibar kupata uongozi wenye ridhaa ya wananchi, na sio kama ilivyo sasa serikali kuwa iliyojiweka baada ya maamuzi ya wananchi kuhujumiwa.
Kuhusu asili ya Mapinduzi, imeelezwa kuwa CUF inatambua Mapinduzi ya 12 Januari, 1964 yanahusu Wazanzibari wote na malengo yake makuu kuelezwa na kufafanuliwa vyema kupitia Dikrii Na. 6 ya mwaka 1964 iliyopitishwa na Baraza la Mapinduzi.
Katika Dikrii hiyo, malengo yanatajwa kwamba ni kuleta usawa, umoja na maridhiano baina ya Wazanzibari wote na kupiga vita aina zote za ubaguzi.
Taarifa imesema kwa kuwa tayari umma wa Wazanzibari umetangaziwa kwamba kuanzia Januari 2 kutakuwa na s hughuli mbalimbali zinazolenga maadhimishio ya Mapinduzi na hatimaye kama ilivyo desturi, kilele chake kufikiwa Januari 12, 2016 kwenye Uwanja wa Amaan, “viongozi wa CUF hawatoshiriki ratiba walizopangiwa mpaka pale chaguo la wananchi wa Zanzibar walilolifanya tarehe 25 Oktoba, 2015 litakapoheshimiwa.”
CUF inasikitisha sherehe za mara hii zinafanyika wakati nchi na watu wake wema wapo katika mtihani mkubwa kufuatia kitendo cha mtu mmoja, Jecha Salim Jecha, kuamua kwa utashi wake na waliomtuma, kuiingiza nchi katika msukosuko na taharuki kwa kudai eti ameufuta uchaguzi mkuu wa tarehe 25 Oktoba, 2015 na matokeo yake.
“… Amevunja Katiba, amevunja Sheria ya Uchaguzi na amevunja hata maadili ya kazi yake, (hivyo) mara hii nchi yetu itaadhimisha Mapinduzi huku Serikali ikiwa inaongozwa na viongozi wasiokuwa na uhalali na ridhaa ya wananchi,” imesema taarifa ya CUF iliyosainiwa na Mansour Yussuf Himid, Mshauri wa Katibu Mkuu wa chama.
Taarifa imesema kwamba ni msimamo wa CUF tangu hapo kuwa hakikubaliani na uamuzi huo wa mtu mmoja kujinyakulia mamlaka ya wananchi wa Zanzibar yaliyowekwa kikatiba, na kwa msingi huohuo, “tunapenda kutumia fursa hii kuwaeleza wananchi wa Zanzibar kwamba viongozi wetu hawatoshiriki katika shughuli walizopangiwa katika ratiba ya sherehe hizi.”
Chama kimetoa sababu nne za kufikia uamuzi huo wa viongozi wake kutoshiriki sherehe za mwaka 2016. Sababu hizo ni zifuatazo:
  • Kwa mujibu wa Katiba ya Zanzibar ya mwaka 1984 (Toleo la 2010), Ibara ya 28, Ibara ya 42(2), Ibara ya 48(b), Ibara ya 90(1) na Ibara ya 92(1) Serikali iliyokuwepo madarakani na Baraza la Wawakilishi lililokuwepo katika kipindi cha miaka mitano iliyopita (2010 – 2015) vilimaliza muda wake wa uongozi tarehe 2 Novemba, 2015 kwa upande wa Serikali na tarehe 12 Novemba, 2015 kwa upande wa Baraza la Wawakilishi. Kwa sasa, hatuna viongozi wenye uhalali wa kikatiba kuweza kutekeleza majukumu ya kiserikali. Kwa hivyo, kushiriki katika ratiba hizo kwa kutumia nafasi ambazo hazina uhalali tena wa kikatiba ni kwenda kinyume na dhamira ya waasisi wa Mapinduzi, jambo ambalo hatuko tayari kulifanya.
  • Kiutaratibu, kilele cha sherehe huongozwa na Rais ambaye yupo kikatiba. Kwa mara ya kwanza tokea tarehe 12 Januari 1964, sherehe za miaka 52 zitaongozwa na Rais ambaye ameshamaliza muda wake wa uongozi kikatiba na ambaye hana uhalali na ridhaa ya wananchi wa Zanzibar. Kushiriki katika sherehe hizo ni kuhalalisha kipindi cha uongozi ambacho hakipo tena kikatiba. Maalim Seif Sharif Hamad na viongozi wenziwe ndani ya Chama waliokuweko Serikalini hadi tarehe 2 Novemba, 2015 hawako tayari kuhalalisha uvunjaji wa Katiba ya Zanzibar ambayo ndiyo sheria kuu ya nchi.
  • Viongozi wa CUF wakiongozwa na Maalim Seif Sharif Hamad wanaamini katika msingi mkuu wa Mapinduzi ya tarehe 12 Januari, 1964 chini ya uongozi wa Baba wa Taifa la Zanzibar, Marehemu Sheikh Abeid Amani Karume, ambao ni kuleta utawala wenye ridhaa ya wananchi walio wengi. Msingi huo umewekwa wazi na kutiliwa nguvu na Katiba ya Zanzibar ya 1984 (Toleo la 2010) kupitia Ibara ya 9(2)(a) ambapo inaelezwa kwamba, “Mamlaka ya kuendesha nchi ni ya wananchi wenyewe ambapo nguvu na uwezo wote wa Serikali kufuatana na Katiba utatoka kwa wananchi wenyewe.” Mamlaka hayo ya wananchi yalitekelezwa tarehe 25 Oktoba, 2015 kwa kuwachagua viongozi watakaoongoza Serikali yao kwa miaka mitano ijayo. Kitendo chochote cha kupindua mamlaka hayo ya wananchi ni kwenda kinyume na misingi ya Mapinduzi na misingi iliyowekwa na Baba wa Taifa la Zanzibar, Marehemu Sheikh Abeid Amani Karume. CUF hatuko tayari kushiriki katika kuisaliti misingi hiyo na kuisaliti dhamira ya Mzee Karume.
  • Sherehe za kuadhimisha Mapinduzi ya tarehe 12 Januari, 1964 zina lengo la kukumbuka malengo ya Mapinduzi hayo na dhamira ya waasisi wake wakiongozwa na Marehemu Sheikh Abeid Amani Karume katika kusimamia utawala wenye ridhaa ya wananchi walio wengi. Kuzitumia sherehe za Mapinduzi kuhalalisha utawala usio na ridhaa ya wananchi wa Zanzibar na ambao haupo kikatiba ni usaliti mkubwa wa dhamira ya kuwepo kumbukumbu hiyo. CUF hatuko tayari kuwa sehemu ya usaliti huo.
CUF inafanya uamuzi huo wakati mgombea wake anayepigania haki ya kukabidhiwa mamlaka kutokana na ushindi alioupata, Maalim Seif, amekuwa akikutana kwa faragha na viongozi wa kitaifa wa Zanzibar akiwemo Dk. Ali Mohamed Shein, ambaye anashikilia uongozi wa serikali inayopingwa uhalali wake.
Viongozi wengine wanaokutana ni marais wastaafu Ali Hassan Mwinyi, Dk. Salmin Amour Juma na Dk. Amani Abeid Karume, pamoja na Balozi Seif Ali Iddi.
Pamoja na vikao hivyo vilivyofikia tisa, hakuna taarifa inayotolewa kwa umma na haijulikani ni lini vitakwisha. Hivi karibuni, Dk. Shein alipokuwa akieleza mazungumzo yake na Rais Dk. John Magufuli wa Tanzania, alisema mazungumzo yatakapomalizika umma utajulishwa matokeo.
Oktoba 28, Jecha alitangaza kufuta uchaguzi mzima kwa madai ya kuwepo matatizo yaliyoutia doa, wakati huo akiwa ameshatangaza zaidi ya asilimia 70 ya kura za urais ikiwa ni majimbo 33 kati ya 54.
Viongozi wa CCM wamekuwa wakishikilia kuwa kutafanyika uchaguzi wa marudio, wakirejea tamko la Jecha alipotangaza kufuta uchaguzi. Tume ya Uchaguzi Zanzibar haijatangaza tarehe ya uchaguzi wa marudio huku kipindi cha siku 90 kilichotajwa kikiwa kinamalizika.

Chanzo: Mwanahalisi Online

Seif rais Zanzibar, maandalizi ya kutangazwa yaiva

[​IMG]

                                Mgombea wa Urais Zanzibar kwa tiketi ya CUF, Maalim SEif Shariff Hamad


USHINDI wa Maalim Seif Shariff Hamad katika uchaguzi mkuu wa Zanzibar uliofanyika Oktoba 25, ungali salama. Anaandika Jabir Idrissa
MAWIO limeelezwa kuwa ushindi huo utadhihirishwa kabla ya Zanzibar kufikia kilele cha maadhimisho ya miaka 51 ya Mapinduzi.
Taarifa zinasema viongozi wa kitaifa, wakiwemo marais wastaafu Zanzibar, ambao wamekuwa wakikutana na Maalim Seif, Ikulu ya Zanzibar, wanakaribia kukamilisha utaratibu wa kuwezesha kiongozi huyo kutangazwa mshindi wa uchaguzi huo.
“Hili halina utata wowote. Nakuhakikishia wanakaribia kuona mantiki na kuelewana; utaratibu wa kumtangaza Maalim Seif utatolewa wakati muafaka,” amesema mwanadiplomasia kutoka moja ya mataifa ya Ulaya.
Amesema kwa kadri anavyofahamu, maendeleo ya mazungumzo hayo yanayomhusisha pia Rais Dk. Ali Mohamed Shein, katika siku za karibuni, yamejikita katika kupata uhakika kuwa serikali mpya itaundwa kwa kuzingatia matakwa ya sheria na katiba.
Lakini amesema, hata suala hilo halijawa tatizo kwa kuwa mfumo wa kuunda serikali umesukwa vema katika Katiba ya Zanzibar ya Mwaka 1984.
“Kama unavyojua mfumo wa serikali utakuwa uleule wa Serikali ya Umoja wa Kitaifa na kwa matokeo ya uchaguzi vyama vya CCM na CUF ndivyo vitaunda serikali mpya,” alisema.
Mwanabalozi huyo aliulizwa na mwandishi jinsi anavyoona hali ya kisiasa kwa sasa na hasa kuhusu mgogoro uliotokana na uchaguzi.
Mgogoro wa sasa Zanzibar ulitokana na uchaguzi mkuu kufutwa kiubabe na Mwenyekiti wa Tume ya Uchaguzi Zanzibar (ZEC), Jecha Salim Jecha.
Jecha alifuta uchaguzi kwa tangazo lililorushwa na Shirika la Utangazaji Zanzibar (ZBC) mchana wa Oktoba 28.
Wakati huo tayari Jecha alikuwa ameshatangaza kura za majimbo 33, akibakiza majimbo 21 tu.
Mwandishi alilenga kupata msimamo wa Jumuiya ya Kimataifa kuhusu kauli tata za viongozi wa juu wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) Zanzibar.
Mwishoni mwa wiki iliyopita, Katibu wa Itikadi na Uenezi wa CCM Zanzibar, Waride Bakari Jabu aliwataka wana-CCM kujiandaa kwa uchaguzi wa marudio aliosema utafanyika “wakati utakapowadia.”
Hata hivyo, kwa mujibu wa vyanzo mbalimbali vya habari ndani ya CCM, Serikali ya Mapinduzi na Serikali ya Muungano, hakutakuwa na uchaguzi wowote bali utakuwepo utaratibu wa kumtangaza mshindi.
Chanzo katika CCM kimesema, “Hili liko wazi, mshindi wa uchaguzi ule ni Maalim Seif wa CUF ambaye naweza kusema amefanikiwa kusimamia ushindi wake huo na hoja zake hazishindiki. Nakwambia atatangazwa siku chache zijazo.”
Kiongozi huyo ambaye aliomba asitajwe jina gazetini, amemsifia Maalim Seif kwa kubaki mtulivu wakati wote akijadiliana na viongozi wenzake ambao wote ni kutoka CCM.
Katibu Mkuu huyo wa CUF na mwanasiasa ambaye amekuwa akilalamika kuhujumiwa mara zote akigombea urais, amekuwa akishiriki mazungumzo na marais wastaafu.
Marais hao ni Ali Hassan Mwinyi, Dk. Salmin Amour Juma, Amani Abeid Karume na Dk. Shein. Makamu wa Pili wa Rais, Balozi Seif Ali Iddi naye amehudhuria mazungumzo hayo.
Dalili za kuwepo muafaka katika majadiliano zimeonekana hivi karibuni pale Dk. Shein, aliyekuwa akigombea urais kwa mara ya pili, na Maalim Seif walipokutana na Rais mpya wa Tanzania, Dk. John Magufuli katika nyakati tofauti.
Wote walisikika wakisema majadiliano yao yanaendelea vizuri, lakini Dk. Magufuli akieleza waandishi wa habari nje ya ofisi yake Ikulu baada ya kukutana na Maalim Seif kuwa, “amenihakikishia wanaendelea vizuri na nimemtaka wakamalize majadiliano yao na apige kazi.”
Dk. Shein alipotoka nje ya maongezi na Dk. Magufuli aliwaambia waandishi wa habari kuwa mazungumzo yanaendelea vizuri na yatakapomalizika, watatoa taarifa kwa umma kuwaeleza maafikiano yaliyofikiwa.
Taarifa zilizopatikana baadaye zinasema moja ya mambo ambayo Dk. Shein alitakiwa kuyafanya baada ya hapo, ni kukutana na Kamati Maalum ya NEC-CCM, kuwaeleza maendeleo ya vikao na viongozi wenzake vinavyofanyika Ikulu.
Jumapili iliyopita, MAWIO lilielezwa kile kilichotokea katika kikao kilichofanyika Ofisi Kuu za CCM Kisiwandui mjini Zanzibar kilichoandaliwa kwa ajili ya Dk. Shein kutoa taarifa yake.
Katika kikao, Dk. Shein “alitoa taarifa yake na taarifa yenyewe kujadiliwa vizuri” mpaka kikao kilipomalizika yapata saa 9.30 alasiri.
Dk. Shein aliondoka na Makamu wa Rais wa Tanzania, Samia Suluhu Hassan, mara baada ya kumaliza kikao.
Lakini baada ya viongozi hao wakuu kuondoka ukumbini, baadhi ya wajumbe waliobaki walianza kudai kuwa hawakubaliani na mapatano na kwamba wanataka uchaguzi urudiwe.
Gazeti hili limeambiwa baada ya Dk. Shein kuondoka Kisiwandui, Balozi Seif alifuatana na baadhi ya viongozi kwenda Ofisi ya Mkoa wa Mjini Magharibi, iliyoko Amani, ambako walifanya mjadala ulioibua kilichoitwa “kauli za chuki” zikimlenga Maalim Seif.
Kwa kuzingatia aliyoyasema Dk. Shein, baadhi ya viongozi walionekana wakifuta machozi kwa kilichoelezwa ni “kutoamini kwao kuwa CUF itapishwa kuongoza serikali mpya.”
Akijibu hoja ya kurudia uchaguzi ambayo wananchi wengi wameonesha kuipinga, Kaimu Mkurugenzi wa Habari na Mawasiliano na Umma wa CUF, Ismail Jussa Ladhu amesema kurudia uchaguzi siyo chaguo la wananchi.
Aliwaambia waandishi wa habari mgogoro wa Zanzibar ni wa kutengeneza, uliolenga kuchanganya wananchi na kuwapora ushindi wao. Ametaka wananchi wapuuze kauli za kurudia uchaguzi.
“CUF inawahakikishia Wazanzibari kwamba haitotetereka; itasimamia kwa dhati maamuzi waliyoyafanya kwa njia za kidemokrasia kupitia uchaguzi mkuu na italinda chaguo lao la Rais wa Zanzibar, Wawakilishi na Madiwani wao,” alisema Jussa.
Amepongeza wananchi kwa kuonesha “ukomavu wa hali ya juu wa kisiasa na kuendelea kutunza amani na utulivu wakati wakisubiri matokeo ya kazi kubwa waliyoifanya tarehe 25 Oktoba ambayo inaashiria ujenzi wa Zanzibar Mpya.”
Ni msimamo wa CUF kuwa Maalim Seif alishinda uchaguzi kwa zaidi ya kura 25,000.
Kwamba CUF ilipata viti 27 vya uwakilishi. Kwamba CCM ilishindwa kupata kiti kisiwani Pemba. Kwamba CUF ilitwaa viti tisa Unguja.

Source: Mwanahalisi Online